
Serikali ina uwezo wa
kugundua barabara iiliyojengwa chini ya kiwango kwa kukagua miradi inayotekelezwa
wakati wote wa ujenzi wa miradi hiyo hata baada ya kukamilika kabla ya muda wa
ukaguzi wa mwisho kupita.
Hayo yamesemwa na
Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Edwin Ngonyani
alipokuwa akijibu swali la Miza Bakari Haji Mbunge wa Viti Maalum lililohoji
kama Serikali inaweza kugundua ni barabara ngapi zilizotengenezwa chini ya
kiwango nchini.
Mhandisi Ngonyani
alizitaja barabara zilizojengwa kwa kiwango cha lami ambazo zilikuwa matatizo
mbalimbali kabla ya muda uliotarajiwa kuwa ni pamoja na Kilwa ambayo inaanzia
Mbagala Rangi Tatu hadi Bendera Tatu, Sekenke hadi Shelui, Kyamorwa hadi Buzirayombo na Nangurukuru hadi Mbwemukulu.
Barabara hizo zilipokamilika
yalijitokeza matatizo mbalimbali kabla ya muda uliotarajiwa yanayotokana na
mapungufu kwenye ubora kama mashimo katika barabara hizo na kuharibika kwa
tabaka mbili za juu.
Mhandisi Ngonyani
amesema kuwa ujenzi wa barabara hutengenezwa kwa kuzingatia mikataba kati ya
TANROADS na Mkandarasi na kati ya TANROADS na Mhandisi Msimamizi na viwango
vinavyotakiwa kwenye ujenzi wa mradi huo wa barabara vimetajwa kwenye mkataba
husika.
“Endapo kunatokea
tatizo lolote kuhusu ubora wa kazi, kwa mfano barabara kujengwa chini ya
kiwango, vipengele vya mkataba husika vitatumika kubaini nani aliyesababisha
mapungufu hayo kati ya Mkandarasi, Mhandisi Msimamizi au mwajiri na hatimaye
kuwajibika” alisema Mhandisi Ngonyani.
Katika kudhibiti
nidhamu ya kuheshimu mikataba, Mhandisi Ngonyani alisema kuwa kutokana na
mapungufu yaliyojitokeza katika mradi wa ujenzi wa barabara husika hatua
zilichukuliwa kulingana na vipengele vya mikataba husika na Mkandarasi wa
miradi hiyo walirekebisha mapungufu yaliyojitokeza katika barabara hizo kwa
gharama zao wenyewe.
Wingi wa magari nao
umeainishwa kuwa ni sababu nyingine ambayo inasababisha uharibifu wa barabara
kutokana na wingi wa magari makubwa ya mizigo yanayotumia ekseli zenye tairi
moja.
Ili kuhakikisha
uthibiti wa uzito wa magari, Serikali inafanya utaratibu wa kufanya mabadiliko
ya kanuni za usalama barabarani za mwaka 2001 ziweze kuoana na Sheria ya
Uthibiti wa uzito wa magari ya Jumuiya ya Afrika ya Mashariki ambayo imeweka kiwango
cha uzito wa tani 8.5 kwenye ekseli zenye tairi moja.
Akijibu swali la
Mbunge wa Nanyumbu Mhe. Dua William Nkurua aliyehoji ni lini Serikali itatekeleza
miradi ya barabara wilaya ya Nanyumbu, Mhandisi Ngonyani alisema kuwa Wakala wa
Barabara Tanzania imekamilisha upembuzi yakinifu na usanifu wa kina wa barabara
ya Nangomba hadi Nanyumbu hatua ambayo itasaidia kujengwa kwa barabara hiyo.
Na Eleuteri Mangi,
MAELEZO, Dodoma