Mratibu
wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Mwakilishi Mkazi wa Shirika la
Maendeleo (UNDP) nchini, Bw. Alvaro Rodriguez akipozi na bango la picha
lenye rangi mbalimbali zinazowakilisha malengo ya dunia 17 kwa Maendeleo
Endelevu wakati wa mdahalo kwenye juma la Umoja wa Mataifa ambalo
linamalizika leo katika maadhimisho ya miaka 70 tangu kuundwa kwa umoja
huo. Mdahalo huo umefanyika katika Ukumbi wa Kimataifa wa Mwalimu
Nyerere jana.(Picha zote na Zainul Mzige wa Modewjiblog).
Na Mwandishi wetu
RAIS
Mstaafu wa awamu ya tatu Benjamin Mkapa ametoa wito wa kufanyika kwa
mabadiliko katika mfumo wa uendeshaji wa Umoja wa Mataifa ili kukidhi
mahitaji ya sasa ya dunia.
Mkapa
alisema hayo jana katika mdahalo kwenye juma la Umoja wa Mataifa ambalo
linamalizika leo katika maadhimisho ya miaka 70 tangu kuundwa kwa umoja
huo. Mdahalo huo umefanyika katika Ukumbi wa Kimataifa wa Mwalimu
Nyerere jana.
Mkapa
ambaye alichukua muda wake mwingi kuelezea na kuangalia maslahi ya
Umoja wa Mataifa kwa dunia na changamoto inazokabiliana nazo, alisema
kwa muda sasa dunia inataka mabadiliko katika uendeshaji wa Umoja huo
lakini wanaonufaika na mfumo wa sasa wamekuwa wagumu kukubali
mabadiliko.
Alisema
kuna mambo sasa yanatokea yanayohatarisha usalama wa mataifa, lakini
hatua zinazopendekezwa zinashindwa kuchukuliwa kutokana na kuendelea
kuwapo kwa tabia ya vita baridi kati ya mataifa makubwa yenye kura ya
veto katika umoja huo.
Alisema
yeye anaungana na watu wengine duniani wanaotaka mabadilio katika Umoja
huo yatakayozingatia jiografia za kisiasa duniani zinazoweza kusaidia
kuinua uwezo wa utekelezaji wa Vyombo vya Umoja wa Mataifa likiwemo
baraza Kuu na Baraza la Usalama.
Mratibu
wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Mwakilishi Mkazi wa Shirika la
Maendeleo (UNDP) nchini, Bw. Alvaro Rodriguez akipozi na Balozi wa
Ireland nchini Tanzania, Mh. Fionnuala Gilsenan.
Alisema
kwamba yapo baadhi ya mataifa na wakazi wa dunia hii ambao wanataka
kuondolewa kwa kura ya turufu inayomilikiwa na mataifa kadha kutokana na
makubaliano ya vita kuu ya pili ya dunia.
Alisema
anafahamu kwamba Afrika inakubaliana na suala hilo kimsingi ingawa lina
changamoto yake kwamba nini kitatokea kama kura hiyo ya turufu
itaondolewa.
Hata
hivyo, Mkapa alisema kwamba masuala ya usalama wa dunia ni nyeti sana
kubaki katika mikono ya watu wachache na kutaka uwezo huo kupewa dunia
kwa kuiwekeza katika sheria ya kimataifa inayotaka uwajibikaji wa pamoja
katika masuala ya usalama.
Alisema
katika kongamano hilo la vijana kwamba Afrika imepitisha azimio la
pamoja Machi 8,2005 la kutaka mabadiliko makubwa katika vyombo vya Umoja
wa Mataifa na umoja wenyewe.