Jul 27, 2015

Wasira, Bulaya waanza kutunishiana misuli

 Waziri wa Chakula na Kilimo Stephen Wasira na Ester Bulaya.  

Dar es Salaam. Waziri wa Kilimo na Chakula, Stephen Wasira amesema hakuwahi kuwa na mvutano wowote na Mbunge wa Viti Maalum, Ester Bulaya, kwa kile alichodai kuwa siyo ‘saizi’ yake kwenye uwanja wa siasa.
Akizungumza na Mwananchi kwa simu jana, Wasira alisema hakuwahi kuvutana na Bulaya na kwamba, kitendo chake cha kuhamia Chadema, kimempotezea mashabiki wengi hususan vijana wa Jimbo la Bunda mkoani Mara.
Hata hivyo, Bulaya alipoulizwa kuhusu hilo alisema kuhama kwake CCM kumemrahisishia kupata wafuasi wengi wakiwamo vijana na wazee huku, akidai kupigiwa simu mara kwa mara za kupongezwa kwa uamuzi wake wa kujiunga Chadema.
“Tangu nilipokuwa CCM, nilikuwa mwakilishi wa vijana na huku Chadema ndiyo kwenyewe, nimeendelea kuiteka Bunda tofauti na awali,” alisema Bulaya.
Alisema hakuwahi kufikiria uamuzi wa kukodi wananchi ili wahudhurie kwenye mikutano yake, bali uhusiano bora kati yake na wakazi wa Bunda ndio uliosababisha umati wa watu kufurika katika mkutano uliofanyika juzi.
Wasira: Bulaya si saizi yangu
Wasira ambaye pia ni Mbunge wa Bunda (CCM), alisema vijana wengi wa jimbo hilo walikuwa wanampenda Bulaya kwa sababu alikuwa CCM ambayo ndiyo chama kilichomlea kisiasa hadi hapo alipofikia hivi sasa.
“Mfano mzuri ni juzi katika mkutano wake uliovunja rekodi ya kuhudhuriwa na watu wengi, wananchi waliletwa kwa malori kutoka sehemu mbalimbali zikiwamo Mwanza na Serengeti,” alisema Wasira ambaye ameomba kuteuliwa kugombea jimbo hilo kwa mara nyingine.
Alidai kuwa Chadema imekuwa ikijinasibu kuwa haiwezi kukodisha wananchi kuhudhuria katika mikutano yao, lakini juzi ilikuwa hivyo.
Akizungumzia hali ya ushindani iliopo kwa wagombea waliojitokeza na kuchukua fomu ya kugombea jimbo la Bunda, Wasira alisema upo kiasi na endapo CCM itampitisha tena, yupo tayari kupambana na yeyote kutoka upinzani hata Bulaya ambaye si saizi yake.
Bulaya: Wasira si saizi yangu
“Kizuri kinajiuza bwana, sikuwa na sababu ya kukodi watu waje kushiriki kwenye mkutano wangu, yeye na chama chake ndio wenye tabia hiyo. Hata hivyo, wataambulia patupu safari hii,” alisema Bulaya.
Bulaya alipouulizwa endapo Chadema ikimpitisha kuwania Bunda ataweza kupambana na mgombea kutoka chama chake za zamani akiwamo Wasira, alijibu:
“Sioni ‘saizi’ yangu kati ya wote waliojitokeza kuchukua fomu ya Bunda, ni bora Wasira akapumzika kwani kizazi chake kwa sasa hakipo.”
Katika hatua nyingine; Wasira amekanusha taarifa kuwa amempiga Mwenyekiti wa CCM, Mkoa wa Mara, Chistopher Sanya.
Wasira alikiri kutokea kwa ubishi wa kawaida kati yake na Sanya, lakini siyo wa kufikia hatua ya kupigana na kwamba, wanaosambaza taarifa hizo wana lengo la kumchafua kisiasa.

chanzo: MWANANCHI