Jul 14, 2015

BARAZA LA USHAURI LA WAZEE CCM KUMBE SI LELEMAMA


6KWANZA kama ilivyo ada nimshukuru Mungu kwa kutufikisha leo tukiwa wazima na afya tele. Mchakato wa kumtafuta mgombea urais kupitia tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) mwaka huu wa 2015 ulikuwa ni mkali na haujawahi kutokea katika historia ya chama hicho tangu wakati wa mfumo wa siasa ya chama kimoja hadi mfumo wa vyama vingi ulipoingia nchini Julai Mosi, 1992.
Ili kupata mgombea mmoja CCM imekuwa ikitumia vikao vyake vitatu, Kamati Kuu (CC), Halmashauri Kuu (NEC) na Mkutano Mkuu (GM) kumpata mwanachama mmoja wa kupeperusha bendera ya chama hicho na ndiye atakayeshindana na wagombea wa kambi ya upinzani ili kuingia ikulu.

Mfumo huo ambao umetumika kumpata mgombea ndani ya chama katika uchaguzi wa mwaka 1995, 2000, 2005 na 2010, mwaka huu umebadilishwa kwani kulikuwa na kikao kingine cha Baraza za Ushauri la chama hicho ambacho kilichuja utitiri wa wagombea na kushauri kabla ya kufikisha kwenye vikao hivyo.
Uzoefu wa washauri hao katika madaraka, hekima, busara na ukongwe katika duru za siasa umesaidia kuchambua wagombea hao na kubakiza wachache  wenye vigezo, taaluma na utendaji na majina yao yakapelekwa Kamati Kuu na hatimaye Mkutano Mkuu wa CCM.
Baraza hilo linaloundwa na Mwenyekiti wake, Rais wa Awamu ya Pili, Mzee Ali Hassan Mwinyi, Katibu, Pius Msekwa na wajumbe wake Rais mstaafu wa Awamu ya Tatu, Benjamin Mkapa, marais wastaafu wa Zanzibar, Amani Abeid Karume na Dk. Salmin Amour pamoja na Mzee John Malecela wamefanya kazi nzuri.
Baraza hilo lililoundwa kwa kanuni za chama mwaka 2012, kwa kutumia uzoefu wa wanachama wake, kumbe huwa linatumika kama chekecheke, dira, mwongozo na kioo cha kupata mgombea safi na bora, tumeona Dodoma.
Wazee hao ambao wamebobea katika medani za siasa walitakiwa kutoa mapendekezo juu ya ubora, uwezo, weledi wa wagombea ndani ya chama ili kusaidia vikao vya chama, kwa kutumia hadidu zao.
Washauri hao wa chama walitakiwa kuwachambua na kuwajadili wagombea wote 38 waliojitokeza kuwania nafasi ya urais kuanzia maisha yao katika jamii, chama na nchi kwa ujumla, kabla majina yao na sifa zao pamoja na vigezo vya kuwapitisha kuyapeleka majina yao mbele ya Kamati Kuu ya CCM.
Kwa wasiojua ni kwamba vikao vya chama vilianza baada ya kupata hadidu za rejea kutoka Baraza la Ushauri la chama, pamoja na nyaraka kutoka Kamati ya Usalama na Maadili na ndipo Kamati Kuu ikafanya uamuzi wa kuteua watangaza nia watano, Januari Makamba, Bernard Membe, Dk. John Magufuli, Amina Salum Ali na Dk. Asha-Rose Migiro.
Kwa ujumla vikao vyote vya mchakato huo havikuwa lelemama, kwanza kutokana na wingi wa wagombea waliojitokeza kuwa na sifa, umahiri, ubora na uwajibikaji uliotukuka, ambapo ni kwa mara ya kwanza wamejitokeza kwa wingi kutoka Bara na Visiwani.
Kazi ya kuchuja wagombea ilikuwa ngumu lakini vikao vilifanya na kubakiza watatu wenye sifa stahiki ambao ni Dk.John Magufuli, Dk. Asha-Rose Migiro na Amina Salum Ali.
Umakini wao katika kuteua wagombea bora kutoka miongoni mwa idadi hiyo kubwa ya watangaza nia ambayo ni kubwa mara mara nne ya wale 11 waliowania urais mwaka 2005, watakumbwa na Watanzania kwa kitendo hicho cha ushujaa cha kukivusha chama salama.
Naamini baraza hilo la wazee lilikuwa likimtegemea Mungu ili kuwasaidia kuangalia uwezo wa mgombea wa kuongoza, taaluma yake ili kuwapa Watanzania rais bora wa awamu ya tano atakayepokea  mikoba ya Rais Jakaya Kikwete mara baada ya Uchaguzi Mkuu utakapofanyika Oktoba 25, mwaka huu ambaye amejulikana kuwa ni Dk. John Pombe Magufuli aliyepata kura 2104 sawa na asilimia 87.1.
Kilichobaki ni wana CCM wote kuungana na kuondoa makundi ili ushindi upatikane na Dk. Magufuli awe rais, anayeng’ang’ania makundi hatufai, atupishe.
Jipu limepasuka, siwezi kuwa adui kwa kusema ukweli. 

GPL