Mwanaharakati John Masweta akiwa kwenye geti kuu la Makao Makuu ya Jiji la Mwanza
Barua ya shukrani kwa Kampuni ya Tanzania Environment & Conservation (TECO) inayomilikiwa na Masweta.
John Masweta akiongea na wananchi kwenye geti kuu la Makao Makuu ya Jiji la Mwanza jana.
Cheti alichopatiwa Mwanaharakati John Masweta.
Na Johnson James, Mwanza
MKURUGENZI wa Jiji la
Mwanza, Halifa Hassan Hida ameingia katika kashfa nzito baada ya
mwanaharakati aliyefahamika kwa jina la John Masweta kutinga kwenye geti
kuu la Makao Makuu ya Jiji la Mwanza jana huku akiwa amevaa gunia
kumshinikiza mkurugenzi huyo amlipe shilingi 1,600,000 aliyopewa kama
zawadi na uongozi wa mkoa na mkurugenzi huyo kushindwa kuilipa fedha
hiyo kwa wakati.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Mwanza kwenye lango kuu la
kuingia ofisi za jiji hilo, Masweta alisema kuwa yeye ni Mwanzilishi na
Mkurugenzi wa Kampuni ya Tanzania Environment & Conservation (TECO)
aliyejitolea kwa zaidi ya miaka 20 kupanda miti na amekuwa akipewa tuzo
mbalimbali kutokana na kazi hiyo na kuweza kuliokoa taifa katika
majanga ya jangwa.
Masweta ameendelea kufafanua kuwa katika kuhakikisha analisaidia
taifa, amepanda miti katika maeneo mbalimbali jijini Mwanza na wakati
akiendelea kupanda miti hiyo akawa amepatiwa tuzo ya mwanaharakati bora
kwa kutunza mazingira iliyoambatana na fedha taslimu shilingi milioni
moja na laki sita lakini cha kushangaza mkurugenzi amekataa kutoa fedha
hiyo na badala yake amempatia cheti tu bila kumpatia na fedha.
Katika hatua nyingine, Masweta ameendelea kusema kuwa yeye hakupanda
miti kwa lengo la kulipwa na taifa bali alipanda miti ili kuliondoa
taifa katika janga la kukumbwa na jangwa lakini cha kushangaza kila
anapotiwa moyo kwa kupatiwa fedha kidogo, fedha hiyo huishia mikononi
mwa watu wengine ambao hawana huruma na maisha yake.
Hata hivyo, Masweta alikuwa na mabango yaliyoandikwa ujumbe
mbalimbali kama Toa nguvu zako kwa kulitumikia taifa, uwe faida kwa
jamii na taifa, onea huruma tumbo lako kula mpaka sisimizi, Udhalimu wa
Mkurugenzi wa Jiji la Mwanza haukubaliki.
Masweta amesema kuwa hatoki kwenye lango hilo hadi pale mkurugenzi huyo atakapompatia kiasi hicho cha fedha anazodai.
Aidha Masweta ametoa rai kwa raia kwa kusema kuwa yeye ni mgonjwa wa
kisukari na hajanywa maji yoyote tokea asubuhi endapo akifariki basi
wafahamu kwamba aliyesababisha kifo chake ni Mkurugenzi wa Jiji la
Mwanza kutokana na kuwa na nia ya kudhulumu haki za wenzake.
GPL