Nov 12, 2014

Maelfu Ya Wananchi Wamtakia Afya Njema Rais Kikwete.....Jana Aliondolewa Bandeji, Hali yake inazidi Kuimarika


HALI ya afya ya Rais Jakaya Kikwete imeendelea kuimarika kwa kasi na jana alizungumza kwa simu na uongozi wa juu wa Tanzania kwa mara ya kwanza tangu afanyiwe upasuaji wa tezi dume Jumamosi iliyopita.
 
Alizungumza na Makamu wa Rais, Dk Mohammed Gharib Bilal, Rais wa Zanzibar, Dk Ali Mohammed Shein na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, lakini pia alikuwa anawasiliana na mamia kwa mamia ya wananchi na kujibu ujumbe mfupi wa maandishi (SMS) wa kumpa pole, kumtakia heri na nafuu ya haraka, ambao amekuwa anatumiwa na wananchi tangu mwishoni mwa wiki.
 
Tangu alipofanyiwa upasuaji wa tezi dume Jumamosi iliyopita kwenye Hospitali ya Johns Hopkins, Baltimore, Jimbo la Maryland, Marekani, Rais Kikwete amepokea mamia kwa mamia ya SMS zikimpa pole na kumtakia nafuu ya haraka.
 
Rais Kikwete bado anaendelea kujibu SMS hizo za wananchi ambao wamemtumia. Wenye SMS hizo wametakiwa kuendelea kusubiri majibu yake kwa sababu anakusudia kujibu SMS zote ambazo ametumiwa.
 
Katika hatua nyingine, madaktari wanaoendelea kumtibu Rais Kikwete, jana waliondoa bendeji kwenye sehemu ambako alifanyiwa upasuaji, wakieleza kuwa hali yake inaendelea vizuri na anapata nafuu kwa kasi nzuri.
 
Italia yaguswa
Nayo Serikali ya Italia imemtakia afya njema Rais Kikwete na kumuombea apone haraka na arejee katika shughuli zake mapema baada ya upasuaji wa tezi dume mwishoni mwa wiki.
 
Salamu hizo zimewasilishwa kwa Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Dk Rehema Nchimbi na Balozi wa Italia nchini, Luigi Scotto wakati alipomtembelea Mkuu wa Mkoa ofisini kwake, ambapo pia alipata fursa ya kutembelea Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma.
 
Balozi huyo alisema Serikali ya Italia imeguswa na afya ya Rais Kikwete na inamtakia apone haraka ili arejee katika kuendeleza harakati za kuwatumikia wananchi wake.
 
Pia alisema Italia itaendelea kuisaidia Tanzania katika miradi yote inayofadhiliwa na Serikali ya nchi hiyo, ikiwemo Mradi wa afya wa magonjwa yanayoambukizwa hususani Ukimwi na Kifua Kikuu kupitia kwa wajawazito yaani “Afya ya mama na mtoto” mradi unaofanyika katika Hospitali ya Rufaa ya mkoa wa Dodoma na Kituo cha Afya cha Makole.
 
Akipokea salamu hizo kwa niaba ya serikali, Dk Rehema Nchimbi, alimpongeza Balozi wa Italia na serikali yake kwa moyo wa kiungwana na upendo kwa watu wa Tanzania na hasa kutokana na kuguswa na afya ya Rais Kikwete.
 
Pia, aliishukuru serikali ya Italia kwa misaada mingi inayoisaidia Tanzania hususani kupitia Mradi wa afya ya Mama na Mtoto, misaada ya elimu na matibabu ya magonjwa yanayoambukiza kupitia wajawazito.